×
Mada hii inazungumzia: masharti nane ya hijabu ya mwanamke wa kiislam, pia imezungumzia dalili katika Quraan na sunna juu ya hijabu ya mwanamke na uwajibu wa mwanamke kukaa nyumbani.

    MASHARTI NANE YA HIJABU

    [Swahili- Kiswahili سواحيلي -]

    Imekusanywa na kuandikwa na:

    Yunus Kanuni Ngenda.

    —™

    Imehakikiwa na:

    Yasini Twaha Hassani.

    Kimerejewa na:

    Abubakari Shabani Rukonkwa.

    الشروط الثمانية للحجاب

    كتبه :

    يونس كنون نغندا

    مراجعة :

    أبوبكر شعبان ركونكوا

    ياسين طه حسن

    MASHARTI NANE YA HIJABU.

    Utangulizi:

    Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe wote, na rehma na amani zimwendee kiongozi wa umma huu Mtume wetu Muhammad (s.a.w) na watu wake na Maswahaba zake wote,! Amma baad.

    Mwanamke ameamrishwa kubakia nyumbani kwake ila kwa dharura tu na akitoka anatakiwa awe amejifunika na kujisitiri vizuri kwa hijaab iliyokamilika kisheria inayopaswa kutimizwa, nayo ni mavazi yanayotakiwa yatimize masharti nane zifuatazo:

    1. Mwili wote ufunikwe isipokuwa uso na viganja vya mikono.[Maulamaa wengine wameona hata uso na mikono pia ifunikwe].

    2. Nguo isiwe yenye mapambo.

    3. Lazima iwe nzito kiasi isiwe yenye kuonyesha mwili.

    4. Lazima iwe yenye kupwaya na sio ya kubana hata ikaonyesha mwili wake.

    5. Asijitie manukato.

    6. Isishabihi vazi la kiume.

    7. Isishabihi mavazi ya kikafiri

    8. Isiwe ya kujionyesha, maana kwamba isiwe kwa ajili ya kiburi kuwa ni vazi bora kuliko la mwengine.

    Amri ya kubakia nyumbani ni Anaposema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):

    ((وَقَرْنَ فِي بُيُوتِكُنَّ))

    ((Na kaeni majumbani kwenu)) [Al-Ahzaab: 33].

    Kwa jinsi iliyvokuwa ni muhimu mwanamke kubakia nyumbani, hata Swalah yake tumeambiwa kuwa ni bora kwake kuswali nyumbani kuliko kwenda Msikitini.

    Na aliporuhusu wanawake kwa kuwakataza Maswahaba wasiwazuie kwenda kuswali misikitini, na walipokuwa wakihudhuria, alipendelea mlango mmoja uwe kwa ajili ya kuingia wanawake:

    عن ابن عمر رضي الله عنهما قال : قال رسول الله صلى الله عليه وسلم: (( لو تركنا هذا الباب للنساء)) . قال نافع : فلم يدخل منه ابن عمر حتى مات" أخرجه أبو داود بسند صحيح

    Kutoka kwa Ibn 'Umar (Radhiya Allaahu 'anhuma) kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Tungeliuacha huu mlango kwa ajili ya wanawake)). Kasema Naafi': "Hakuingia tena Ibn 'Umar mlango huo mpaka kufariki kwake". [Abu Daawuwd kwa isnaad Swahiyh]

    وعن أم سلمة رضي الله عنها قالت : "أن النساء في عهد رسول الله صلى الله عليه وسلم كن إذا سلمن من المكتوبة قمن وثبت رسول الله صلى الله عليه وسلم ومن صلى من الرجال ما شاء الله فإذا قام رسول الله صلى الله عليه وسلم قام الرجال" أخرجه البخاري . قال ابن شهاب (وهو الزهري ): فأرى والله أعلم أن مكثه لكي ينفذ النساء قبل أن يدركهن من انصرف من القوم .

    Kutoka kwa Ummu Salamah (Radhiya Allaahu 'anha) ambaye amesema: "Wanawake katika zama za Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) walikuwa wakimaliza kuswali Swalah za fardh waliondoka, na akabaki Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na wanaume waliojaaliwa kuswali, kisha alipoinuka Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na wao waliinuka" [Al-Bukhaariy na Muslim]. Amesema Ibn Shihaab (ambaye ni Az-Zuhriy) naona kuwa na Allaah Ndiye Mjuzi zaidi kuwa kubaki kwake Mtume msikitini ni kuachia nafasi ya wanawake kuondoka kwanza kabla ya wanaume.

    Vile vile, itakapombidi mwanamke kutoka nje kwa dharura basi ahakikishe kuwa anatekeleza maamrisho ya Mola wake katika hali hiyo, kama tulivyotaja kuhusu hijaab na pia katika maongezi akaze sauti yake.

    ((فَلَا تَخْضَعْنَ بِالْقَوْلِ فَيَطْمَعَ الَّذِي فِي قَلْبِهِ مَرَضٌ وَقُلْنَ قَوْلًا مَّعْرُوفًا))

    ((Basi msiregeze sauti zenu, akaingia tamaa mwenye maradhi katika moyo wake. Na semeni maneno mema)) [Al-Ahzaab: 32].

    Hali Inayoruhusu Kuchanganyika

    Kuna baadhi ya hali za dharura zinazoruhusika kuchanganyika, na mfano wa hali hizo ni kama imetokea mwanamke kuharibikiwa safarini, kupotea, kutaka kudhuriwa na watu au kuvunjiwa heshima na ikabidi kumuokoa na kumsindikiza hadi penye amani au palipo watu wake, kupatwa na ajali kukawa hakuna wanawake wa kumsaidia ila wanaume tu, na hali nyinginezo mbalimbali za dharura kama za matibabu ikiwa hakuna madaktari wa kike n.k.

    Katika Haram (Makkah)

    Baadhi ya watu wanatoa hoja ya Msikiti wa Makkah wanapoona kwenye matelevisheni au kwa waliojaaliwa kufika kuwa kule kuna mchanganyiko wa wanaume na wanawake. Wengi wanashindwa kuelewa kuwa hali ile ya dharura inayosababisha vile si hoja ya kumfanya Muislamu kuruhusika kuchanganyika kwani huko kuna ulazima wa kutekeleza Twawaaf na haiwezekani kuwatenga wanawake katika ibada hii kutokana na hali ilivyo, watu kuhitajika kufanya Twawaaf wanapoingia tu Haram, umbali wanaotoka watu nchi kwa nchi, na muda wa ibada hiyo na kutowezekana kupangika zamu ya utekelezaji wa ibada hiyo kwa wanaume na wanawake ndio kukapatikana dharura hiyo.

    Pamoja na kuwepo hali hiyo na ugumu huo wa kuwatenganisha wanawake na wanaume kwenye Twawaaf, askari waliomo Msikitini hapo wanajaribu sana kuwatenganisha wanawake na wanaume katika kuswali ingawa wengi huwa wakaidi.

    Katika Kazi

    Ikiwa kuna dharura ya kufanya kazi na ikasababisha kuchanganyika, kwani katika kufanya kazi mfano biashara kutakuweko wanawake na wanaume, ila lazima izingatiwa sheria isemavyo na kutekeleza inavyopasa na kuepukana na makatazo.

    Kuhudumia Wageni

    Wanapokuja wageni wa mume au jamaa zake mke lakini ambao sio mahaarim wake, anaweza kuwahudumia kwa kuwatayarishia chakula kama kuwapelekea, muhimu aweko mumewe. Hii ni kutokana na dalili ifuatayo:

    لما عرَّسَ أبو أُسَيد الساعِدِيُّ دعا النبيَّ صلى الله عليه وسلم وأصحابَهُ فما صنَع لهم طعاماً ولا قدم إليهم إلا امرأتُهُ أمُّ أُسيد، بَلَّتْ (وفي رواية: أنقعت) تَمَراتٍ في تَوْر من حجارةٍ منَ الليل، فلما فَرَغَ النبيُّ صلى الله عليه وسلم من الطعام أماثَتْه له فسقَتْهُ تتْحِفُه بذلك. (فَكَانَتِ امْرَأَتُهُ يَوْمَئِذٍ خَادِمَهُمْ. وَهْيَ الْعَرُوسُ)

    Abu Asyad As-Saa'idiy alipooa, alimualika Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) pamoja na Maswahaba zake. Hakuna aliyetayarisha chakula au kuwahudumia isipokuwa mkewe Ummu Asyad. Aliroweka tende katika bakuli la udongo usiku uliopita. Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alipomaliza kula, alimpakulia na kumtunikia, hivyo mkewe akawa ndiye mwenye kuwahudumia wageni na alikuwa ndiye bi harusi. [Al-Bukhaariy, Muslim na wengineo].

    Katika Kusaidia Kazi Za Jihaad

    Inafaa wanawake kusaidia katika kazi kama hizo kama kuwatibu waliojeruhiwa, au kuwapelekea maji n.k. kwani hivyo walifanya wanawake zama za Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam). Na kazi kama hizo kwa ajili ya maslahi wa Waislamu.

    Swafiyyah bint 'Abdul-Mutwalib, Shangazi yake Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alishiriki katika kuwapiga makafiri na kumkinga Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam), pia aliweza kumuua Myahudi kwa kumkata kichwa chake hata wakaingiwa na khofu Mayahudi waliotaka kuvamia kambi waliyoachwa wanawake, watoto na wazee kwa kudhania kwamba kuna mwanamume hivyo hawakuthubutu kuwasogelea.

    Vile vile katika kushirikiana kutekeleza kazi za Dini kama kufunza watu, kuwapatia misaada wanayohitaji, kutoa ushauri mbali mbali n.k. maana kuna baadhi ya wanawake wamejaaliwa kuwa na busara na hikma katika mambo haya. Vile vile uwezo kwa kusaidia kwa njia yoyote ile, kama ni wa kifedha, kielimu n.k.

    Katika Sehemu Za Kutafuta Elimu

    Wanaruhusiwa wanawake kuhudhuria madarsa yanayotolewa na wanaume ikiwa mashuleni, Misikitini, vyuoni, au kwenye kumbi, ila lazima kuweko mtengano baina yao, ama kwa kuweka pazia baina yao au wanawake wakae nyuma ya wanaume.

    Hali kadhalika baadhi ya wanawake wanaweza kutoa mafunzo na wakasikilizwa na wanaume ila lazima pia shari’ah zake za stara zitekelezwe kama tulivyotaja juu. Mama wa Waumini 'Aaishah (Radhiya Allaahu 'anha) alikuwa akiwafunza Maswahaba walipomjia kwa masuala mbali mbali ya Dini yao.

    Wa Allaahu A’alam