×
Mada hii inazungumzia: Bishara wanayopewa na Allah watu wenye tawhid na msimamo wa kweli katika imani na ucha Mungu.

    KUWA NA TAWHID YA KWELI NI SABABU YA KUPATA MWISHO MWEMA

    Imeandaliwa na: Yunus Kanuni Ngenda

    Imepitiwa na: Abubakari Shabani Rukonkwa

    Sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe wote, na rehma na amani zimwendee kiongozi wa umma huu Mtume wetu Muhammad (s.a.w) na watu wake na Maswahaba zake wote,! Amma baad.

    Muislamu anapokuwa na msimamo katika tawhid, na imani, na ucha Mungu, hubashiriwa Pepo wakati anapofikwa na mauti. Anasema Mwenyezi Mungu mtukufu:

    إِنَّ الَّذِينَ قَالُوا رَبُّنَا اللَّـهُ ثُمَّ اسْتَقَامُوا تَتَنَزَّلُ عَلَيْهِمُ الْمَلَائِكَةُ أَلَّا تَخَافُوا وَلَا تَحْزَنُوا وَأَبْشِرُوا بِالْجَنَّةِ الَّتِي كُنتُمْ تُوعَدُونَ ﴿٣٠﴾ نَحْنُ أَوْلِيَاؤُكُمْ فِي الْحَيَاةِ الدُّنْيَا وَفِي الْآخِرَةِ ۖ وَلَكُمْ فِيهَا مَا تَشْتَهِي أَنفُسُكُمْ وَلَكُمْ فِيهَا مَا تَدَّعُونَ ﴿٣١﴾ نُزُلًا مِّنْ غَفُورٍ رَّحِيمٍ ﴿٣٢﴾

    Hakika wale waliosema: “Rabbuna (Mola) wetu ni Allaah.” Kisha wakanyooka (wakawa na msimamo); Malaika huwateremkia (wakati wa kutolewa roho kuwaambia) kwamba: “Msikhofu, na wala msihuzunike, na pokeeni bishara njema ya Jannah ambayo mlikuwa mkiahidiwa (kwayo). “Sisi ni marafiki walinzi wenu katika uhai wa dunia na katika Aakhirah. Na mtapata humo yale yanayotamani nafsi zenu, na mtapata humo yale mnatayoyaomba. “Ni mapokezi kutoka kwa Ghafuwrir-Rahiym (Mwingi wa kughufuria, Mwenye kurehemu).” [Fusw-Swilat: 30-32].

    Na amesema Mwenyezi Mungu mtukufu:

    إِنَّ الَّذِينَ قَالُوا رَبُّنَا اللَّهُ ثُمَّ اسْتَقَامُوا فَلا خَوْفٌ عَلَيْهِمْ وَلا هُمْ يَحْزَنُونَ ** أُوْلَئِكَ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ خَالِدِينَ فِيهَا جَزَاء بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ

    Hakika walio sema: “Mola wetu Mlezi ni Mwenyezi Mungu; kisha wakatengenea (wakawa na msimamo), hawatakuwa na khofu, wala hawatahuzunika. Hao ndio watu wa Peponi, watadumu humo, kuwa ni malipo kwa waliyo kuwa wakiyatenda.” [Surat Ahqaaf: 13-14]

    Ukitafakari kwa umakini Aya hizo tukufu, utatambua ya kwamba mtu kusema “RABBUNA LLAH” pekee! haitoshi kwake yeye kupata bishara njema, isipokuwa lazima neno hilo liambatane na:

    1.Tauhid ya dhati.

    2.Imani ya kweli.

    3-Msimamo ulio madhubuti.

    5.Na matendo yaliyo mema.

    Ndiyo maana Mwenyezi Mungu mtukufu mwisho wa Aya anasema:

    “Hao ndio watu wa Peponi, watadumu humo, kuwa ni malipo kwa waliyo kuwa wakiyatenda.” [Surat Ahqaaf: 13-14]

    Tunamuomba Mwenyezi Mungu mtukufu atujaalie tuwe na tauhid ya kweli katika nyoyo zetu, na atufishe hali ya kuwa ni waislam wenye imani thabiti, na atuwezeshe kwa rehma zake tuweze kutenda matendo yaliyo mema ili tupate mwisho mwema, na atufufue Mola wetu pamoja na Mtume wetu Muhammad (s.a.w) siku ya Kiyama, Ameen!

    وصلى الله على محمد وعلى آله وصحبه وسام.